Tayari serikali ya Pretoria imetuma ujumbe mjini Hague nchini Uholanzi kwenda kufuatilia kesi hiyo.
Afrika Kusini ilifungua kesi dhidi ya Israel mwishoni mwa mwezi Disemba mwaka uliomalizika, baada ya takriban miezi mitatu ya vita vya maangamizi ya umati vya Israel dhidi ya Wapalestina huko Gaza.
Katika nyaraka za kesi, Afrika Kusini imesema hatua za Israel ni "mauaji ya kimbari kwa sababu zina nia ya kuleta uharibifu wa sehemu kubwa ya kundi la taifa, rangi na kaumu ya Palestina."
ICJ ilisikiliza kesi hiyo dhidi ya jinai za kivita za Wazayuni huko Gaza mnamo tarehe 11 na 12 mwezi huu wa Januari. Mbali na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran, nchi nyingine kadhaa zimetangaza kuunga mkono hatua hiyo ya kihistoria ya Afrika Kusini ya kuuburuza kizimbani utawala wa Kizayuni kutokana na mauji yake ya kizazi cha Wapalestina hasa wa Ukanda wa Gaza.
Baada ya kusikiliza pande zote kwenye kesi hiyo, Rais wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki, Joan Donoghue alisema mahakama hiyo ya kimataifa ya mjini The Hague itatoa uamuzi wake haraka iwezekanavyo.
Hata hivyo Ofisi ya Mrajisi ya Mahakama ya ICJ haijatoa maelezo yoyote kufikia sasa kuhusu ratiba ya kutolewa uamuzi kuhusu faili hilo la Afrika Kusini dhidi ya utawala wa Kizayuni ambao unaendelea kuua watoto na wanawake wa Gaza.
3486946