Sambamba na kupanua ujenzi haramu wa vitongoji katika mji wa Quds (Jerusalem) na maeneo mengine, utawala wa Kizayuni wa Israel unalenga kupora na kuiba maeneo zaidi ya ardhi za Palestina na kuligawanya vipande vipande eneo la Ukingo wa Magharibi ili kuzitenganisha sehemu mbalimbali za eneo hilo, lengo likiwa ni kuimarisha ukaliaji kwa mabavu ardhi za Palestina na kukamilisha mchakato wa kuyayahudisha maeneo yote ya ardhi hizo.
Kwa mujibu wa taarifa, shirika la ujenzi la utawala wa muda wa Kizayuni katika Ukingo wa Magharibi limetangaza kuwa, kamati ndogo ya ujenzi wa vitongozi iliyo chini ya baraza kuu la mipango la Tel Aviv imepanga kuanzisha ujenzi wa nyumba mpya zipatazo 3,988 kwa ajili ya walowezi wa kizayuni.
Mradi huo umetangazwa sambamba na ripoti zilizotolewa na vyombo vya habari kuhusu uwezekano wa rais Joe Biden wa Marekani kutembelea ardhi za Palestina zinazokaliwa kwa mabavu, zilizopachikwa jina la Israel na hatua zinazochukuliwa na Tel Aviv za kujaribu kuandaa kikao maalum na viongozi wa nchi za Kiarabu.
Ripoti za kuaminika zinaeleza kuwa, utawala wa Kizayuni umefanya mazungumzo ya moja kwa moja na Marekani kuhusiana na upitishaji wa mpango huo.
Hii ni katika hali ambayo Desemba 2016, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio 2334, ambalo liliutaka utawala wa Kizayuni wa Israel ukomeshe ujenzi haramu wa vitongoji katika ardhi za Palestina