Katika mkutano huo wa Jumatatu mjini Tehran, Rais wa Iran ameashiria katika mazungumzo hayo manufaa ya pamoja ya pande mbili, matukio ya kieneo na kimataifa na kusema kuwa,hii leo kuna haja ya kuandaliwa mipango ya muda mrefu na ya pande zote kwa ajili ya ustawi na kuimarishwa zaidi uhusiano wa Tehran na Damascus.
Rais Ibrahim Raisi amesema pia kuwa, uwepo usio wa kisheria wa vikosi vya kigeni katika eneo na katika ardhi ya Syria ni jambo hatarishi kwa usalama na uthabiti wa eneo na kuongeza kuwa, kundi la kigaidi la Daesh limeanzishwa na kulelewa na Marekani, na hii leo uwepo wa Daesh na Washington katika eneo lolote lile katika ukanda huu kutauletea hasara kubwa usalama, uthabiti na amani ya mataifa ya eneo hili.
Kadhalika Rais Ibrahim Rasi amesistiza udharura wa kuheshimiwa mamlaka na ardhi yote ya Syria na kueleza kwamba, kupuuza hilo ni jambo ambalo halikubaliki kwa namna yoyote ile na bila shaka wananchi wa Syria katu hawawezi kulivumilia hilo.
Kwa upande wake, Faisal Mekdad, Waziri wa Mashauri ya Kigeni wa Syria sambamba na kumkabidhi Rais wa Iran ujumbe kutoka kwa Rais Bashar al-Assad na kumwalika kuitembelea Syria amesema kuwa, Damascus imeazimia kwa dhati kutumia uwezo wake wote kwa ajili ya kuimarisha uhusiano wake na Tehran.