Kwa mujibu wa mwandishi wa Shirika la Habari za Qur’an la Kimataifa IQNA, Nadzim Johan wa 'Jumuiya ya Watumizi Bidhaa Waislamu Malaysia (PPIM) amesema: "Hii ni kesi ya kushtua sana kwani imeripotiwa katika kiwanda kikubwa ambacho kina mfumo mzuri wa viwango na hata kina cheti cha Bidhaa Halali. Kwa hivyo jambo kama hili halipaswi kuibuka." Katika mahojiano na gazeti la Rakyat Post siku ya Jumanne Mei 27, Johan alisema: "Sisi Waislamu tunahisi tumehadaiwa, kudhulumiwa na tumpepata dhiki na mfadhaiko mkubwa baada ya kujua kile tulichokula."
Utata kuhusu chokleti hizo za Cadbury uliibuka pale vipande vidogo vidogo vya nyama ya nguruwe ilipopatikana katika chokoleti mbili kufuatia uchunguzi uliofanywa na Wizara ya Afya ya Malaysia.
Kufuatia ropiti hiyo, Idara ya Ustawi wa Kiislamu Malaysia (Jakim) ilibatilisha mara moja cheti cha 'Halal' cha Cadbury na kusema bidhaa zote za shirika hilo zitaondolewa madukani. Aidha mashirika ya Kiislamu Malaysia yametoa wito wa kususiwa bidhaa zote zinazotengenezwa na Cadbury.
Vile vile kuna mpango wa kuwasilisha mashtaka mahakamani dhidi ya Shirika la Cadbury kwa hila zake hizo za kuwahadaa Waislamu.
Waislamu ni zaidi ya asilimia 60 ya watu wote milioni 26 nchini Malaysia
Nyama na bidhaa zote za nguruwe ni haramu na najisi kwa mujibu wa mafundisho ya dini tukufu ya Kiislamu.
1411579