IQNA

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu

Trump hana ustahiki wa kubadilishana naye ujumbe, hatutafanya mazungumzo na Marekani

15:30 - June 13, 2019
Habari ID: 3472000
TEHRAN (IQNA)- Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amesema: "Jamhuri ya Kiislamu ya Iran haiimaini Marekani hata kidogo na uzoefu mchungu wa mazungumzo yaliyotangulia na Marekani katika fremu ya JCPOA kamwe hautarudiwa tena kwani hakuna taifa lolote huru na lenye akili litakubali kufanya mazungumzo chini ya mashinikizo."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Sayyid Ali Khamenei ameyasema hayo leo asubuhi mjini Tehran alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri Mkuu wa Japan Shinzo Abe (Abe Shinzo).

Mwanzoni mwa mkutano huo, Waziri Mkuu wa Japan alimhutubu Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu Ayatullah Khamenei na kumwambia: "Mimi ninataka kukukabidhi ujumbe kutoka kwa rais wa Marekani."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu naye alimhutubu Waziri Mkuu wa Japan na kumwambia: "Sisi hatuna shaka kuhusu nia yako njema na uzito unaolipa swala hili lakini kuhusu kile ulichokinukulu kutoka kwa rais wa Marekani nasema kuwa, Trump hana ustahiki kwa kubadilishana naye ujumbe wowote na pia sitamjibu chochote."

Ayatollha Khamenei ameashiria mazungumzo ya waziri mkuu wa Japan kuwa Trump amemefahamisa kuwa "Marekani haina lengo la kuupindua utawala wa Iran" na kusema: "Tatizo letu na Marekani si maudhui ya kuupindua utawala kwani hata wakiwa na lengo kama hilo hawawezi kulitekeleza kama ambavyo katika kipindi cha miaka 40 iliyopita, marais waliotangulia Marekani walijaribu kuiangamiza Jamhuri ya Kiislamu ya Iran lakini walishindwa."

Kiongozi Muadhamu ameashiria sehemu nyingine ya kauli ya Waziri Mkuu wa Japan kuwa Marekani ina azma ya kuizuia Iran kuunda silaha za nyuklia na kuongeza kuwa: "Sisi tunapinga silaha za nyuklia na nimetoa fatuwa ya kisheria kuhusu uharamu wa silaha za nyuklia. Lakini fahamu kuwa, iwapo sisi tungekuwa na kusudio la kuunda silaha za nyuklia, Marekani haingweza kufanya chochote kutuzuia na hivyo Marekani kutotoa idhini ya hilo si kizuizi."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu ameashiria mkondo wa mazungumzo na Marekani katika fremu ya JCPOA na kusema: "Punde baada ya mapatano ya nyuklia, mtu wa kwanza kukiuka mapatano hayo alikuwa ni Obama, Huyo ni yule yule ambaye aliomba kufanya mazungumzo na Iran na hata akatuma mjumbe mpatanishi."

Ayatullah Khamenei ameashiria sehemu nyingine ya kauli ya Waziri Mkuu wa Japan kuwa Trump amesema: "Mazungumzo na Marekani yatapelekea Iran istawi" na kusisitiza kuwa: "Tumeweza kustawi kwa uwezo wake Mwenyezi Mungu, na pasina kuwepo mazungumzo na Marekani na pamoja na kuwepo vikwazo."

Kiongozi Muadhamu wa Mapinduzi ya Kiislamu amekaribisha pendekezo la Waziri Mkuu wa Japan la kuimarisha uhusiano na Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na kusema: "Japan ni nchi muhumu barani Asia, na iwapo inataka kuimarisha uhusiano na Iran inapaswa kuonyesha irada yake kamili kama ambavyo baadhi ya nchi muhimu zimeonyesha.

Kwa upande wake, Shinzo Abe ameashiria mazungumzo yake akiwa mjini Tehran na kuelezea matumaini kuwa, mazungumzo hayo yataandaa mazingira ya kushirikiana zaidi.

3819076

captcha