IQNA

Ayatullah Araki ampigia simu Sheikh Zakzaky nchini India

19:38 - August 15, 2019
Habari ID: 3472085
TEHRAN (IQNA) - Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu amefanya mazungumzo ya simu na Kiongozi wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria (IMN) Sheikh Ibrahim Zakzaky aliyepelekwa India kwa ajili ya matibabu.

Katika mazungumzo hayo yaliyohusu mwenendo wa matibabu ya Sheikh Zakzaky, Ayatullah Muhsin Araki ameeleza wasiwasi wake kuhusu hali ya kiafya ya Sheikh Zakzaky na kusema kuwa: Jamhuri ya Kiislamu ya Iran na Jumuiya ya Kukurubisha Pamoja Madhehebu za Kiislamu itafanya juhudi zote kuhakikisha kwamba, mwanazuoni huyo wa Kiislamu anapata matibabu.

Ayatullah Araki ambaye yuko nchini India kwa safari rasmi, alijaribu kupata idhini ya kumtembelea Sheikh Zakzaki hospitalini bila mafanikia na hatiamye aliweza kuzungumza naye kwa njia ya simu mapema leo Alhamisi.

Ayatullah Araki amesema kuwa, hali ya kiroho ya Sheikh Zakzaky ni nzuri sana.

Kwa upande wake Sheikh Ibrahim Zakzaky ameishukuru Jamhuri ya Kiislamu kwa juhudi kubwa zilizofanyika na kusema kuwa hadi sasa mwenendo wa awamu za matibabu yake bado haujaanza.

Baadhi ya ripoti kutoka India zinasema kuwa, Sheikh Zakzaky amewekwa katika mazingira ya usimamizi mkali, hali ambayo amesema ina taathira hasi kwa mwenendo wa matibabu yake.

Mawakili wanaomtetea kiongozi huyo wa Harakati ya Kiislamu ya Nigeria wanasema jicho la kulia la Sheikh Zakzaky limepoteza nguvu za kuona na kuna uwezekano jicho lake jingine likapata tatizo kama hilo.

Wameongeza kuwa vilevile kuna risasi kadhaa zilizosalia katika mwili wa mwanazuoni huyo baada ya kushambuliwa na jeshi la Nigeria mwaka 2015 katika mji wa Zaria.

Binti wa Sheikh Zakzaky Suhaila Zakzaky amesema kuwa baba yake anasumbuliwa na matatizo mengi ya kiafya na kimwili likiwemo shinikizo la damu la kiwango cha juu.

Sheikh Zakzaky aliwasili New Delhi nchini India juzi kwa ajili ya matibabu. Mahakama ya Nigeria Jumatatu iliyopita ilimruhusu Sheikh Zakzaky na mkewe kwenda India kwa ajili ya matibabu.

Sheikh Ibrahim Zakzaky pamoja na mkewe walitiwa nguvuni na askari wa jeshi la Nigeria Desemba 13, 2015 katika shambulio na uvamizi uliofanywa na askari hao dhidi ya Huseiniya ya mji wa Zaria nchini humo.

Siku hiyo askari wa jeshi la Nigeria waliwafyatulia risasi watu waliokuwa wamejumuika kwenye kituo hicho cha kidini na mbele ya nyumba ya msomi huyo na kuwaua shahidi mamia miongoni mwao wakiwemo watoto wake watatu wa  kiume. Sheikh Zakzaky pamoja na mke wake walijeruhiwa vibaya sana katika tukio hilo na wiki hii hatimaye utawala wa Nigeria uliwaruhusu kupata matibabu.

3835105

captcha